KIGOMA YATANGAZA MAFANIKIO UDHIBITI WA EBOLA
MKOA Kigoma unaelezwa kupiga hatua kubwa katika kudhibiti kuingia kwa ugonjwa wa Ebola ambao kwa sasa umesababisha idadi kubwa ya vifo katika nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na kwamba kwa sasa hakuna mgonjwa aliyeripotiwa mkoani humo.
MKUU wa mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro akizungumza katika kikao cha wadau wa afya kutathmini hatua zilizochukuliwa kudhibiti ugonjwa huo alisema kuwa pamoja na mafanikio hayo hatua Zaidi za kudhibiti hali hiyo zimeendelea kutekelezwa.
Katika hotuba iliyotolewa kwa niaba yake na Mkuu wa wilaya Kigoma, Dk.Rashid Chuachua alisema kuwa malengo na mikakati iliyowekwa imefanya kazi na kuufanya mkoa huo kuwa salama hadi sasa ambapo ametoa wito kwa wataalam wa afya na wadau mbalimbali kuhakikisha hatua Zaidi zinachukuliwa kuhakikisha ugonjwa huo hauingii mkoani humo sambamba na kuwataka kila moja kutoa taarifa anapoona kuna mtu mwenye dalili ya mgonjwa.
Akitoa taarifa kwa wajumbe wa kikao hicho hatua mbalimbali zilizochukuliwa na timu ya afya ya mkoa, Mratibu wa magonjwa ya mlipuko mkoa Kigoma, Albert Paschal alisema kuwa hatua muhimu za kudhibiti ugonjwa huo zimetekelezwa na kufanikisha kuufanya mkoa huo kubaki salama hadi sasa ikiwemo kutoa elimu kwa wahudumu wa afya mkoani humo.




