WANANCHI ZAIDI YA ELFU KUMI BUKOBA WAONDOKANA NA ADHA YA MAJI
Na Anold Deogratias Matukio Daima Media Kagera
Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) mkoa wa Kagera umekamilisha uchimbaji na ujenzi wa visima 10 vya kuchotea maji katika kata nne za wilaya ya Bukoba, kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 500, hatua inayotarajiwa kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama kufikia asilimia 74 na kunufaisha zaidi ya wananchi 10,000.
Akizungumza na waandishi wa habari meneja wa RUWASA wilaya ya Bukoba Mhandisi Evaristo Mgaya amesema kuwa visima vyote kumi zimekamilika na vimeanza kutoa maji ambapo kila kisima kitakuwa na uwezo wa kuhudumia wananchi zaidi ya 1,000.
“visima vyote vimekamilika vinatoa huduma kwa wananchi kila kisima kitahudumia wananchi elfu moja na kwa watu wa maeneo ya jirani na visima hivyo wananchi wanapata huduma bora za maji safi na salama”
Kwa upande wake meneja wa mradi wa Rukoma na Rubale Moshi Issac amewaomba wananchi kuendelea kutumia hudumu zao na kuwaunga mkono katika utoaji wa huduma ya maji kwa kuunganisha maji kwenye makazi yao.
“nitoe wito kwa wananchi waendelee kutumia huduma zetu na waunganishe maji kwenye nyumba zao ili kuondokana na adha ya wananchi wengi kwenda sehemu moja kwa ajili ya kupata huduma ya maji lakini pia itawezesha kuokoa muda”
Nao baadhi ya wananchi wa akiwemo Diocres Willibard Mkazi wa Kyaitoke ameshukuru uwepo wa mradi huo katika maeneo yao na kueleza kuwa hapo awali walikuwa na shida kubwa ya maji na ilikuwa inawatesa hasa wanafunzi waliokuwa wanalazimika kutembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo nyakati za kiangazi.


