HALMASHAURI ZATAKIWA KUIMARISHA HUDUMA YA MSINDIKIZAJI WA MJAMZITO
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
HALMASHAURI za mkoa Kigoma kupitia idara za afya za halmashauri hizo zimetakiwa kuimarisha mpango wa Mama wajawazito kuwa na wasindikizaji ili kuchochea jamii kwenda kwenye vituo rasmi vya kutoa huduma za afya unapofika wakati wa kujifungua.
Kaimu Mganga Mkuu wa mkoa Kigoma, Nice Msendo alisema hayo wakati Shirika lisilo la kiserikali la thamani uhai likifunga mradi wa Mama msindikizaji ambao ulitekelezwa mkoani Kigoma kuanzia mwaka 2007 na sasa mpango huo unaachwa kuendelezwa na serikali.
Msendo alisema kuwa wadau wa maendeleo katika sekta ya afya mkoa Kigoma wamekuwa na mchango mkubwa katika kusaidia huduma za afya ikiwemo masuala ya afya ya mama mjamzito na watoto na majukumu ambayo ni ya serikali hivyo miradi kama hiyo inapofikia mwisho ni lazima waganga wakuu wa wilaya na timu za huduma za afya za mkoa na wilaya kuiendeleza.



