KITIKI KULETA MAPINDUZI YA KILIMO KWA WAKULIMA WADOGO
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
SHIRIKA la Chakula la Umoja Mataifa (WFP) limekabidhi zana za kilimo zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 50 kwa vikundi vitano vya wakulima katika wilaya za Kasulu, Kibondo na Kakonko ili kubadilisha kilimo cha wanachama wa vikundi kufanya kilimo cha biashara na kuondokana na kilimo cha kujikimu.
Vikundi hivyo vimekabidhiwa zana hizo baada ya kushinda wazo la uandishi bora wa miradi ya kilimo biashara kwa mwaka 2025/2026 kupitia mradi wa kilimo tija Kigoma (KITIKI) unaotekelezwa na WFP kupitia ufadhili wa Shirika la maendeleo la serikali ya Korea Kusini (KOICA) ambapo mwaka wa fedha 2024/2025 kiasi cha shilingi milioni 93 kilitolewa.
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo Meneja wa KITIKI (WFP), HYOYEOL LEE alisema kuwa sambamba na kukabidhi zana hizo kwa vikundi hivyo vitano pia wakulima binafsi saba wamefanikiwa kupata zana za kilimo ikiwemo vifaa na mashine za umwagiliaji,mashine za kupandia, kuwekea mbolea na kupukuchulia mahindi.
Kwa upande wake Mwakilishi wa Meneja wa Kanda ya Magharibi wa Shirika la World Vision, Eric Kidohela alisema kuwa kutekelezwa kwa mradi huo na kutolewa kwa vifaa hivyo kutaleta mabadiliko makubwa ya kilimo kwa wanufaika hao kufanya kilimo chao kuwa cha biashara na kuwa chenye tija kubwa.



