SIRRO ANG'AKA MRADI SOKO LA KATONGA KUCHELEWA
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
MKUU wa mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro amemtaka mkandarasi anayejenga Mwalo wa Katonga Manispaa ya Kigoma Ujiji kutoka kampuni ya M/S Asabhi Co. Ltd. na Pioneer Builders Ltd kufika ofisini kwake mjini Kigoma leo Februari 26 ili aweze kutoa maelezo ya kuridhisha kuhusiana na kuchelewa kutekelezwa kwa mradi huo unaopaswa kukamilika April mwaka huu.
Balozi Sirro alisema hayo alipotembelea na kukagua mradi huo akieleza kupata taarifa za kusuasua kwa mradi huo unaotekelezwa sambamba na mradi wa soko la Mwanga Manispaa ya Kigoma Ujiji na kusema kuwa hakubaliani na hali ya utekelezaji wa mradi huo.
Akiwa kwenye mradi huo Mkuu huyo wa mkoa akiambatana na Mkuu wa wilaya Kigoma, Rashid Chuachua na watendaji wenngine wa serikali alishuhudia mradi huo wa Mwalo wa Katonga ukiwa kwenye hatua ya Msingi hali inayodhihirisha kuwa hautaweza weza kukamilika mwezi April mwaka huu.
Akitoa maelezo kuhusu mradi huo Msimamizi wa mradi huo kutoka Wakala wa barabara za mjini na Vijijini (TARURA) wilaya ya Kigoma, Elius Mutapima alisema kuwa kwa sasa mradi umefikia asilimia 45 na kwamba mradi ulikuwa na changamoto ya kuongezeka kwa maji ya ziwa hivyo kulazimika kufanya usanifu upya
Mwenyekiti wa Umoja wa wavuvi mkoa Kigoma, Francis John alisema kuwa wamelisubiri soko hilo kwa muda mrefu maana limesababisha kuhamisha shughuli zao kwenda maeneo ambayo hayako vizuri kiutendaji lakini kibiashara hivyo wanatamani soko liishe haraka warudi maeneo hayo.
Mwisho.




