MBARONI KWA WIZI WA SOLAR ZA MRADI WA MAJI
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
POLISI mkoani Kigoma imewakamata watu watatu wakazi wa kijiji cha Mwamila wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma wakituhumiwa kuiba vifaa vya umeme jua (Solar Panel) vilivyokuwa vikitumika kwenye mradi wa maji kwenye kijiji hicho.
Kamanda wa polisi mkoa Kigoma,Filemon Makungu akitoa taarifa kwa waandishi wa habari mjini Kigoma alisema kuwa watu hao walikamatwa wakati polisi wakifanya doria na ndipo walipowakamata watu hao wakiwa na vifaa hivyo na wapoulizwa hawakuwa na majibu ya kutosheleza.
Kamanda Makungu alisema kuwa watuhumiwa walikamatwa na Solar Panel sita aina ya Day Loff zenye ukubwa wa watt 335 na kwamba watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani upelelezi utakapokamilika.
Katika tukio lingine Kamanda Makungu alisema kuwa polisi wakiwa doria walikamata mkazi mmoja wa Mtaa wa Katubuka Manispaa ya Kigoma Ujiji akiwa ni vifaa na mali mbalimbali zinazodhaniwa kuwa za wizi kutokana na kutokuwa na nyaraka za kumiliki mali hizo.
Bila kumtaja jina mtuhumiwa Kamanda huyo wa polisi alisema kuwa katika doria hiyo Mtuhumiwa huyo alikamatwa akiwa na TV tatu ambapo kati yake mbili aina ya Mo Electronics za ukubwa wa nchii 32 na nyingine aina Volton nchi 75 na Radio moja Sabufa aina ya Sea Piano, visimbuzi vitatu vya Azam TV Star Time, simu tisa ikiwemo simu mbili za aina ya Teckno na nyingine saba za Google Pixel, mashuka 17 na doti saba za vitenge vya wax na kwamba mtuhumiwa atafikishwa mahakamani upelelezi ukikamilika.
Mwisho.




