BAJETI MANISPAA KIGOMA UJIJI, KIGOMA DC ZAUNGWA MKONO
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
WAJUMBE wa kamati ya ushauri ya wilaya Kigoma kwa kauli moja wamepitisha makisio ya mapato na matumizi ya Halmashauri ya wilaya Kigoma na Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Katika kikao kilichofanyika Mjini Kigoma chini ya Uenyekiti wa Mkuu wa wilaya Kigoma, Dk.Rashid Chuachua wajumbe hao wameeleza kuwa bajeti hiyo inaonyesha utekelezaji wa wazi wa mipango ya maendeleo ya wananchi itakayofanywa na halmashauri hizo katika kukuza uchumi na kuleta maendeleo.
Akizungumza katika kikao hicho hicho Mwenyekiti wa CCM wilaya Kigoma Vijijini, Halimeshi Mayonga alisema kuwa mapendekezo ya bajeti hiyo ni mazuri lakini changamoto kubwa ni upatikanaji wa fedha zilizoombwa hasa katika kutekeleza miradi ya maendeleo hivyo kuwaomba wabunge wa mkoa Kigoma kushirikiana kuhakikisha bajeti zilizopitishwa katika halmashauri za mkoa Kigoma zinapitishwa na kusimaamia fedha zipatikane.
Mbunge wa jimbio la Kigoma Kaskazini, Kiza Mayeye akichangia kuhusu makisio hayo ya mapato na matumizi ya bajeti hizo za Halmashauri alisema kuwa zinaakisi uhalisia wa kuleta maendeleo kwa mkoa Kigoma na kwamba yeye akishirikiana na wabunge weingine wa mkoa Kigoma wataipigania kuhakikisha bajeti inapitishwa na bunge na fedha za utekelezaji zinatolewa.
Katika bajeti hiyo Halmashauri ya manispaa ya Kigoma Ujiji, inakadiria kukusanya na kutumia kiasi cha shilingi bilioni 44.9 katika mwaka wa fedha wa 2026/2027 Halmashuri ya wilaya Kigoma ikiwa inakadiria kukusanya na kutumia kiasi cha shilingi Bilioni 41 katika mwaka wa fedha wa 2026/2027
Mwisho.