Kwa Habari za kitaifa, Kimataifa, Michezo, Burudani,Uchambuzi na matangazo. Matukio Daima Blog, Ni yetu Sote!
 SHILINGI BILIONI 356 ZATUMIKA KUTEKELEZA MIRADI MOROGORO

SHILINGI BILIONI 356 ZATUMIKA KUTEKELEZA MIRADI MOROGORO


Na Lilian Kasenene, Morogoro

Matukio DaimaApp 

SHILINGI bilioni 356 zimetumika kutekeleza miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Morogoro kwa kipindi cha Novemba 2025 hadi Juni 2026, hatua inayolenga kuboresha na kusogeza huduma bora kwa wananchi.

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Adam Malima alibainisha hayo wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika kikao cha Halmashauri Kuu ya Mkoa ya chama hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Magadu.

Malima amesema fedha hizo zimetokana na vyanzo mbalimbali, ambapo Shilingi bilioni 326 zilitoka Serikali Kuu, Shilingi bilioni 20 ni mapato ya ndani ya Mkoa, huku Shilingi bilioni 10 zikitokana na fedha za wahisani.

Amefafanua kuwa fedha hizo zimesaidia kuboresha sekta mbalimbali zinazogusa maisha ya wananchi, ikiwemo ujenzi na ukarabati wa barabara, nishati ya umeme, maji, afya, elimu, kilimo, maendeleo ya ushirika na mifugo.

“Kwa kipindi cha Novemba 2025 hadi Juni 2026, Mkoa wa Morogoro umetekeleza miradi mbalimbali na kuharimu zaidi ya Shilingi bilioni 356,” amesema Malima.

Sanjali na hayo, Mkuu huyo wa Mkoa alisema Serikali imeendelea kuhakikisha uwepo wa majengo bora katika vituo vya afya pamoja na shule za msingi na sekondari, huku akisisitiza umuhimu wa wataalamu kutoa huduma bora kwa wananchi kwa wakati na kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Joseph Masunga, aliwataka viongozi wa chama na Serikali kutafuta maeneo yenye tija ya kuwekeza, hususan katika sekta ya kilimo, badala ya kuwekeza katika miradi isiyo na tija kiuchumi

Amefafanua kuwa uwekezaji katika majengo ya fremu katika maeneo mbalimbali umekuwa ukitoa mapato madogo, hivyo akahimiza uwekezaji kuelekezwa katika miradi yenye uwezo wa kuongeza kipato na kuchochea maendeleo.

Nao wajumbe wa kikao hicho, akiwemo Katibu wa CCM Wilaya ya Kilosa,Jafari Kunambi, wameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha na kusimamia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

*Mwisho.*

Sponsored ads

Mid 1

Mid2

Ad3