TRA YATOA ZAWADI KWA MAMA WAJAWAZITO, WALIOJIFUNGUA
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
Kuelekea maadhimisho ya miaka 30 tangu kuanzishwa kwake uongozi wa mamlaka ya mapato (TRA) mkoa Kigoma imetoa zawadi kwa mama wajawazito na waliojifungua katika hospitali i ya Mkoa wa Kigoma Maweni.
Hatua hiyo imelenga kuunga mkono huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na kuonesha mshikamano wa taasisi hiyo na jamii kupitia shughuli za uwajibikaji kwa jamii ikithamini mchango wa wanawake hao kama sehemu ya walipa kodi nchini kupitia njia mbalimbali.
Akizungumza wakati wa kukabidhi zawadi hizo, Naibu Kamishna uwezeshaji biashara TRA Makao makuu, Julieth Nyomolelo alisema kuwa zawadi zilizotolewa ikiwa ni kurejesha shukrani kwa jamii ambayo ndiyo msingi wa mafanikio ya mamlaka hiyo sambamba na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana na jamii katika kuboresha ustawi wa wananchi.
Awali Kaimu Mganga Mfawidhi wa hospitali ya mkoa Kigoma Maweni, Lameck Mdengo aliwashukuru TRA kwa zawadi hiyo kwamba imethamini mchango wa kina mama hao katika kuchangia mapato ya serikali sambamba na kuishukuru TRA ambayo mara nyingi imekuwa ikisaidia vifaa na masuala mbalimbali ya uendeshaji wa hospitali hiyo.
Mmoja wa wanawake waliofikiwa na zawadi hizo Zainabu Saidi ambaye alijifungua watoto mapacha alishukuru kwa niaba ya wagonjwa na kina mama wengine ambao walikuwepo hospitalini hapo kwa kuona wanastahili kupata zawadi hizo.
Zawadi zilizotolewa ni pamoja na sabuni za unga za kufulia, maziwa ya kopo, chupi za mkojo za watoto (Baby Diappers).
Mwisho.




