DC KASULU AONYA WANAOWAHIFADHI, KUWATUMIA WAHAMIAJI HARAMU
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanali Isaack Mwakisu amewataka viongozi na wananchi wa wilaya hiyo wanaotaka kuwatumia wakimbizi na raia wa kigeni kutoka Burundi kufuata taratibu za kisheria za kuwapatia vibali vya kuishi na vibali vya kazi vinginevyo watu wote wanaoishi na wageni bila kufuata taratibu watashughulikiwa kisheria.
Mwakisu alisema hayo akizungumza kwenye baraza la madiwani la Halmashauri ya wilaya Kasulu akieleza kuhusu opereshini ya siku 10 iliyofanywa kwa muunganiko wa wa vyombo vyote vya ulinzi na usalama mkoani Kigoma ambayo ameeleza imekuwa na mafanikio makubwa ambapo watu zaidi ya 300 walikamatwa kwa tuhuma za kuishi wilayani humo bila kufuata sheria.
Akizungumza katika kikao hicho Makamu mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya Kasulu, Charles Benjamini aliyekuwa mwenyekiti wa kikao hicho,alisema kuwa baadhi ya viongozi wakiwemo madiwani wamekuwa wakituhumiwa wakiwakingia kifua wahamiaji haramu kutokana na kuishi nao na kuwatumia kwa kazi mbalimbali za kilimo hivyo baada ya maelekezo hayo ya Mkuu wa wilaya , wamekubaliana kushirikiana ili kutokomeza changamoto hiyo.
Baadhi ya madiwani waliohudhuria baraza hilo akiwemo diwani wa kata ya Rungwe Mpya, Venance Kaja alisema kuwa operesheni hiyo itasaidia kupunguza wimbi kubwa la wahamiaji harami ambao wameishi na kufanya kazi bila kufuata taratibu lakini pia wamekuwa wakijihusisha kwenye masuala ya uhalifu.


