DC CHUACHUA AWAONYA WAJASILIAMALI WANAOCHUKUA MIKOPO YA HALMASHAURI
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
MKUU wa wilaya Kigoma Dk.Rashid Chuachua amesema kuwa wajasilimali wanaochukua mikopo kutoka mapato ya ndani ya halmashauri kuhakikisha wanarejesha mikopo yao kwa wakati na kwamba watakaoshindwa kufanya hivyo watakumbana na taratibu ngumu za kisheria.
Chuachua alisema hayo wakati akikabidhi hundi yenye thamani ya shilingi Milioni 211 kwa vikundi 24 vya wajasiliamali vya manispaa ya Kigoma Ujiji ambavyo vimekidhi kupata mkopo kutoka halmashauri hiyo katika robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Mkuu huyo wa wilaya alisema kuwa wajasiliamali wote wanapaswa kuzingatia mikataba ya mikopo yao, kuzingatia malengo ya mikopo lakini pia kuzingatia nidhamu ya pesa wanapofanya shughuli zao za kiuchumi na kukumbuka kwamba wanadeni ambalo wanapaswa kulilipa vinginevyo nidhamu mbaya ya matumizi ya fedha inawatumbukiza kwenye changamoto kubwa ya masuala ya kisheria.
Akizungumza katika hafla hiyo Afisa maendeleo ya jamii wa manispaa ya Kigoma Ujiji, Jabiri Majira alisema kuwa katika awamu hii ya pili yam waka huu wa fedha Halmashauri imetoa kiasi cha shilingi milioni 211 baada ya hapo awali kuwa zimeshatolewa shilingi milioni 619 na kufanya halmashauri kuwa imetoa mikopo ya shilingi milioni 830 hadi sasa.
Kwa upande wake Msimamizi wa mikopo ya Wajasiliamali kutoka Benki ya CRDB kanda ya Magharibi, Editha Soka alisema kuwa kabla ya kutolewa kwa mikopo wamekuwa wakitoa elimu ya fedha na usimamizi wa miradi kwa wajasiliamali sambamba na elimu ya uwekaji akiba ili shughuli zinazofanywa na vikundi vikipata changamoto waweke kuchukua akiba waliyoweka kutatua changamoto zinazojitokeza.
Mwisho.




