VIBANDA VYA BIASHARA KIGOMA UJIJI VYATEKETEA KWA MOTO
May 23, 2026
Na Fadhili Abdallah,Kigoma
MOTO umeteketeza vibanda tisa vya biashara katika soko la Kibirizi kwenye bandari ndogo ya Kibirizi manispaa ya Kigoma Ujiji usiku wa kuamkia Mei 23 mwaka huu ambapo Mkuu wa mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro ametembelea soko hilo na kutoa pole kwa wahanga wa tukio hilo.
Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Kigoma, Michael Maganga akitoa taarifa kwa Mkuu wa mkoa Kigoma alisema kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa moto huo unadaiwa kuanzia kwenye kibanda cha Mama Lishe aliyekuwa akiandaa Maharage katika Mgahawa wake, kisha kuyaacha yakiendelea kuiva na kwenda Nyumbani.
Maganga alisema kuwa Askari wa Zimamoto walifika eneo la tukio majira na kufanikiwa kuudhibiti kabla haujasambaa kwenye vibanda vingine vya Biashara vilivyokuwa vikijishughulisha na uuzaji wa Nguo pamoja na Migahawa.
Mkuu wa mkoa Kigoma, Balozi Simon Sirro alifika kutembelea na kukagua uharibifu na madhara yaliyotokea ambapo alipata nafasi ya kuzungumza na watu mbalimbali waliokuwepo kwenye eneo hilo wakiwemo wahanga waliounguliwa na vibanda vyao.
Akiwa hilo Mkuu huyo wa mkoa ametoa maagizo kwa kikosi cha Zimamoto mkoa Kigoma kufabya uchunguzi wa kina kubaini chanzo na kuchukua hatua za kisheria kwa mtu atakayebainika kusababisha moto huo kwa uzembe huku akieleza kuwa watakutana na viongozi wa mabenki mkoani Kigoma kuona namna wanavyoweza kuwasaidia kupata mikopo nafuu lakini ameomba wenye uwezo wa kufanya wenyewe waendelee na shughuli zao
Mwisho.



