ONGEZEKO KUBWA LA WANUFAIKA WA MIKOPO YA ELIMU YA JUU HADI 292,981
Na Hamida Ramadhan, Matukio Daima Media Dodoma
SERIKALI imetangaza ongezeko la wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu nchini, ambapo idadi yao inatarajiwa kupanda kutoka wanafunzi 252,773 katika mwaka wa fedha 2025/26 hadi kufikia 292,981 mwaka 2026/27.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Adolf Mkenda, alipowasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/27.
Aidha, Serikali itaongeza idadi ya wanufaika wa Samia Scholarship kutoka wanafunzi 2,630 hadi 2,738, ikiwa ni mkakati wa kuwasaidia wanafunzi wenye ufaulu wa juu kuendeleza masomo yao katika ngazi ya elimu ya juu.
Kupitia mpango wa Samia Extended Scholarship, Serikali itaendelea kutoa ufadhili kwa wanafunzi bora wa Kidato cha Sita kujiunga na vyuo vya nje ya nchi, hususan katika fani za sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM).
Vilevile, Serikali inalenga kuimarisha udahili wa wanafunzi 180,000 katika programu mbalimbali za elimu ya juu, pamoja na kuongeza nafasi kwa wanafunzi 24,978 wa stashahada katika fani za sayansi na ufundi.
Kwa ujumla, mkazo utawekwa katika kukuza fani za STEM, zikiwemo sayansi ya data na akili unde (Artificial Intelligence), ili kuandaa wataalamu watakaosaidia kukuza uchumi wa kisasa na wenye ushindani.
