TUMBAKU YAIPATIA NCHI DOLA BILIONI 1.2
Singida,
Zao la tumbaku limeendelea kuonyesha nguvu yake katika kuinua uchumi wa nchi, baada ya kuchangia zaidi ya dola za Marekani bilioni 1.2 katika mzunguko wa fedha nchini msimu wa kilimo 2024/2025, hatua inayodhihirisha nafasi yake kwa wakulima na sekta ya kilimo kwa ujumla.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa mafanikio hayo yametokana na mauzo yaliyofanywa na kampuni za ununuzi wa tumbaku, huku zao hilo likitajwa kuwa tegemeo muhimu kwa wakulima wengi kujipatia kipato kikubwa.
Katika msimu huo, uzalishaji wa tumbaku ulifikia kilo milioni 185.7, kiwango kilichochangia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa mzunguko wa uchumi wa taifa na kuongeza mapato kwa wadau mbalimbali wa sekta hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Tumbaku Tanzania, Stanley Mnozya, alisema hayo wakati wa mkutano wa 23 wa wataalamu wa masoko ya tumbaku ulioanza kufanyika mkoani Singida kwa siku tatu, ukilenga kujadili mafanikio na changamoto za zao hilo.
“Msimu uliopita tulinunua kiasi kikubwa cha tumbaku ambacho hakijawahi kununuliwa tangu uhuru, zaidi ya kilo milioni 185.7, na kuwaingizia wakulima dola milioni 475,” alisema Mnozya.




