Kwa Habari za kitaifa, Kimataifa, Michezo, Burudani,Uchambuzi na matangazo. Matukio Daima Blog, Ni yetu Sote!
MCHENGERWA: MAFANIKIO YA BIMA YA AFYA YAPIMWA NA WANANCHI

MCHENGERWA: MAFANIKIO YA BIMA YA AFYA YAPIMWA NA WANANCHI

 


Na Hamida Ramadhan, Mtukio Daima Media Dodoma

WAZIRI wa Afya, Mohammed Mchengerwa, amesema utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote (BAW) hautapimwa kwa idadi ya matamko au maandiko ya sera, bali kwa namna wananchi wanavyopata huduma za afya katika vituo vilivyopo karibu nao.


 Ameyasema hayo leo Januari 23,2026 wakati wa kikao kazi cha viongozi wa Mikoa, Wilaya na Halmashauri kilichojadili maandalizi ya uzinduzi wa awamu ya kwanza ya mpango huo, akieleza kuwa afya ni eneo la msingi katika maendeleo ya Taifa.


Amesema Serikali imeamua kuanza utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa awamu ili kuimarisha mifumo ya usajili, utoaji huduma na usimamizi wa bima kabla ya kuwahusisha wananchi wote.


"Awamu ya kwanza italenga wananchi wasio na uwezo wakiwemo wazee, watoto, wanawake wajawazito na watu wenye ulemavu, ambao gharama za bima yao zitagharamiwa na Serikali, " Amesema Waziri huyo


Aidha ameeleza kuwa Wakuu wa Mikoa wanabeba dhamana ya moja kwa moja ya kusimamia utekelezaji wa mpango huo katika maeneo yao, huku mafanikio ya kila Mkoa yakitarajiwa kuakisi kiwango cha uongozi na ufuatiliaji.


Amesema  kuwa viongozi wa Wilaya na Halmashauri wanapaswa kuhakikisha usajili wa wananchi unafanyika hadi ngazi ya kata, kijiji na mtaa ili kuondoa mianya ya mwananchi kubaki nje ya mfumo wa bima.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema Serikali inaendelea na maandalizi ya kuanzisha mfumo mmoja wa kitaifa wa kidijitali wa afya utakaounganisha huduma, usimamizi wa bima na udhibiti wa gharama.

" Ubora wa huduma katika vituo vya afya ni kichocheo muhimu cha wananchi kujiunga na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, akisisitiza kuwa huduma kwa mwananchi ni haki na si hisani, " Amesema Waziri Mchengerwa.



Pia Ameeleza kuwa viongozi wanapaswa kuimarisha utoaji wa elimu ya umma kuhusu mpango huo pamoja na kuendelea na zoezi la utambuzi wa kaya zisizo na uwezo.

"Bima ya Afya kwa Wote ni ahadi ya Serikali kwa wananchi wake, na utekelezaji wake unahitaji uwajibikaji wa pamoja ili kuhakikisha kila Mtanzania analindwa dhidi ya gharama za matibabu, " Amesema.

Naye Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa Grace Magembe, amesema Kitita cha Huduma Muhimu kwa awamu ya kwanza kitaanza kutumika tarehe 26 Januari 2026, huku dirisha la usajili kwa makundi yatakayogharamiwa na Serikali likifunguliwa rasmi.


Amesema Tanzania ina zaidi ya kaya milioni 3.9 zisizo na uwezo, lakini kaya zipatazo 931,693 pekee ndizo zilizokwisha tambuliwa. 

"Serikali imewaagiza viongozi wa mikoa, wilaya na halmashauri kushirikiana kikamilifu katika zoezi la utambuzi wa kaya hizo ili kuhakikisha hakuna mwananchi anayebaki nje ya mfumo kwa sababu ya urasimu au uzembe, " Amesema.

Akizungumza kwa niaba ya sekta ya maendeleo ya jamii, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. John Jingu, amesema wataalam wa maendeleo ya jamii wana jukumu la kujenga uelewa na kubadilisha fikra za wananchi ili washiriki kikamilifu katika mpango huo.




Sponsored ads

Mid 1

Mid2

Ad3